Mke wa Rais Magufuli asaidia wazee Chato


Mke wa Rais, Janeth Magufuli amekutana na wazee wasiojiweza wilayani Chato na kutoa misaada ya vyakula ili kuwapunguzia changamoto zinazowakabili.
Janeth amekabidhi msaada huo leo (Julai 7) kwa wazee zaidi ya 400 kutoka kata 23 za Wilaya ya Chato mkoani Geita.
Taarifa ya Ikulu imemkariri Janeth akiitaka jamii, watu binafsi, wadau wa maendeleo na taasisi mbalimbali kushirikiana kuwasaidia wazee nchini.
Amezitaja baadhi ya changamoto zinazowakabili wazee hao kuwa ni chakula, dawa na hata upendo na kuthaminiwa.
“Tunawaomba mnaokaa na wazee muonyeshe upendo, muwasaidie pale wanapohitaji msaada, kama wewe una nguvu basi msaidie hata kuchota maji na kukata kuni kwa kuwa hizo ndiyo baraka zenyewe,” amesema.
Wazee hao wamemshukuru mke wa Rais kwa moyo wa kujitolea na hasa katika kuwasaidia wazee na wasiojiweza.
Wameiomba Serikali kuangalia namna ya kupunguza changamoto zinazowakabili wazee.
Akisoma risala kwa niaba ya wazee hao, Ofisa Maendeleo wa Jamii, Lidiana Kasheku ameeleza namna halmashauri  ilivyojipanga kutatua kero za wazee hao ikiwa ni pamoja na kuanzisha baraza la wazee litakalosaidia kubaini changamoto na aina ya msaada wanaouhitaji.
Amesema pia wamejipanga kutoa kipaumbele kwa wazee katika huduma mbalimbali ikiwemo matibabu.
Msaada uliokabidhiwa ni mchele, unga wa mahindi, mafuta ya chakula, sabuni na maharage.

Wilaya ya Chato ina vijiji 115 vyenye wazee zaidi ya 18,000.
Mke wa Rais Magufuli asaidia wazee Chato Mke wa Rais Magufuli asaidia wazee Chato Reviewed by Erasto Paul on July 07, 2017 Rating: 5

No comments:

Thank you for commenting to Mwanauswahili

Powered by Blogger.