Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah
Kairuki amesema watumishi wa umma walioghushi vyeti watachukuliwa hatua za
kinidhamu.
Kairuki
amesema hayo leo (Julai 11) katika kikao kazi na watumishi na viongozi wa
Halmashauri ya Wilaya ya Temeke, Tarafa ya Mbagala.
Amesema
wote walioghushi vyeti hawapo kazini na wameshafutwa katika orodha ya malipo ya
Serikali.
Waziri
ameelekeza waajiri kuwafuta wote wasiostahili kuwepo katika orodha ya malipo na
wasimsubiri hadi afike katika maeneo yao ya kazi ili kutekeleza agizo hilo.
“Baada ya
uhakiki kukamilika, hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa walioghushi vyeti kwa
kuzingatia sheria, kanuni, utaratibu na miongozo iliyopo katika utumishi wa
umma,” amesema Kairuki kama alivyokaririwa katika taarifa iliyotolewa na
wizara.
Amewataka
waajiri kuhakikisha wanahakiki taarifa za watumishi wapya wanapoajiriwa na wale
wanaohamia ili kujiridhisha kama wana vyeti safi.
“Ni wajibu
wa kila mwajiri kuhakikisha kuwa vyeti vya kila mwajiriwa mpya vinathibitishwa
na mamlaka husika kabla ya kumwajiri na hatimaye kumuingiza kwenye orodha za
malipo ya mshahara kupitia mfumo wa HCMIS na mifumo mingine ya mishahara ya
kitaasisi,” amesema.
Akizungumzia
watumishi wa umma walioajiriwa na sifa za darasa la saba, Kairuki amesema
endapo aliajiriwa kabla ya Mei 20 mwaka 2004 anastahili kuendelea kuwa katika
utumishi wa umma na endapo kajiendeleza abadilishiwe muundo kuendana na sifa za
elimu aliyopata.
Amesema
endapo mtumishi huyo aliajiriwa baada ya Mei 20 mwaka 2004 anatakiwa kuwa na
sifa ya elimu ya kidato cha nne.
Kairuki
pia ametoa ufafanuzi wa kazi inayoendelea inayohusu kuoanisha taarifa za
watumishi na zile za usajili uliofanywa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa
(Nida).
“Uhakiki
huu utaongeza usahihi wa taarifa za watumishi nchini, kudhibiti watumishi hewa,
udanganyifu wa taarifa zinazomhusu mtumishi na kutekeleza azma ya Serikali ya
kuunganisha mifumo ya kimkakati ya Tehama ili ibadilishane taarifa,” amesema.
Katibu
Tawala Mkoa wa Dar e Salaam, Theresia Mbando amempongeza Waziri Kairuki kwa
kuboresha utumishi wa umma.
Mbando
amesema sasa watumishi wa umma waliobaki kazini wameweza kuziba pengo la
waliobainika kuwa na vyeti vya kughushi na kuondolewa kazini.
Walioghushi vyeti kuchukuliwa hatua za kinidhamu.
Reviewed by Erasto Paul
on
July 11, 2017
Rating:
No comments:
Thank you for commenting to Mwanauswahili